MASHAIRI YA CHEKACHEKA-UCHAMBUZI|Vol 01
MWANDISHI-THEOBARD MVUNGI
WACHAPISHAJI - EP & D.LTD
MAUDHUI
DHAMIRA
1. Kutetea Haki
Mshairi anamshauri kiongozi wa nchi aendelee kuwasha moto dhidi ya watu wote wanaodhulumu haki za wengine. Katika shairi la MWINYI UMEWASHA MOTO ANGALIA USIZIMWE, mshairi anasema,
“Tumaini la wanyonge, kwamba ipo serikali,
Ile nchi ya mazonge, ya wenye meno makali,
Wanyang'anyao matonge, wanyonge hawana hali,
Mwinyi ukiwa mkali, ndio raha ya raia.”
2. Demokrasia
Mshairi anapinga mfumo wa chama kimoja. Kwake yeye, mfumo huu, unawanyima watu uhuru wa kutoa maoni yao na kukosoa pale mapungufu yanapojitokea. Shairi hili liitwalo TAIFA WAMELIZIKA liliandikwa kipindi ambacho Tanzania ilikuwa katika mfumo wa chama kimoja. Hata hivyo bado lina uhalisia hasa ukizingatia uminywaji wa demokrasia na uhuru wa vyama vya upinzani leo hii. Mshairi anasema,
“Mezikwa demokrasi, Chama kimoja ndo' ngao
Watu hawana nafasi, kutetea nchi yao
Mawazo ya ukakasi, mawazo ya mtitio…”
3. Mapenzi
Mshairi anaeleza jinsi mapenzi yanavyoweza kumtesa mtu hasa pale unayempenda anaposhindwa kukuelewa. Katika shairi la NJIWA KIUMBE MTINI mshairi anasema,
“Nimejaribu kuongea, ndege awe mkononi,
Yeye juu hurukia, namuomba samahani,
Nyimbo ananiimbia, nyimbo zachoma moyoni,
Basi mie taabani, njiwa akitabasamu.”